Mkuu wa Operesheni wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Simon Siro (54) (pichani), amedai mahakamani kuwa alitoa zuio la kuandamana kwenda Ikulu kwa wanachama wa Baraza la Wanawake (Bawacha) kwa sababu maandamano hayo yangesababisha uvunjifu wa amani.
 
Alitoa madai hayo wakati akitoa ushahidi mbele ya Hakimu Mkazi Janeth Kaluyenda, katika kesi inayomkabili Mwenyekiti wa Bawacha, Halima Mdee na wenzake, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam jana.
 
Alidai baada ya kupitia vigezo vya kiusalama, walibaini kuwa njia waliyotaka kuitumia kufanya maandamano hayo inatumiwa na watu wengi, hivyo alishughulikia mara moja kuzuia maandamano hayo.
 
Akiongozwa na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Tumaini Kweka, shahidi huyo alidai kuwa Oktoba 2, mwaka huu alipokea barua iliyopitia kwa Kamanda wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, kutoka Bawacha wakiomba kufanya maandamano ya amani kwenda Ikulu.
 
“Katika barua hiyo, Bawacha waliomba kufanya maandamano kwenda Ikulu kwa Rais Jakaya Kikwete kumtaka asipokee katiba inayopendekezwa…maandamano hayo yalipangwa kufanyika Oktoba 4, mwaka 2014 saa 3:00 asubuhi,” alidai Siro na kuiomba mahakama ipokee nakala ya barua hiyo kama kielelezo, lakini yakatokea mabishano ya kisheria.
 
Kesi iliahirishwa hadi Machi 3, mwaka huu, ushahidi utakapoendelea kusikilizwa.
 
Katika kesi ya msingi, washitakiwa wanadaiwa Oktoba 4, mwaka 2014, katika Mtaa wa Ufipa, bila kuwa na uhalali walikiuka amri halali ya kutawanyika iliyotolewa na Mrakibu wa Polisi Emmanuel Tille kwa niaba ya Jeshi la Polisi na kwamba, siku hiyo walifanya mkusanyiko usio halali kwa lengo moja la kutembea kwenda ofisi ya Rais Kikwete.

Advertisement

0 comments:

 
Top