Ni wakati mwingine kwa Tanzania kujipanga katika soka baada ya wiki hii Shirikisho la Soka Afrika (CAF) kutangaza ratiba ya kufuzu kwa fainali za Afrika mwaka 2017 (Afcon) na pia fainali za wachezaji wa ligi za ndani (CHAN) za mwaka 2016, ambako Taifa Stars imepangiwa timu ngumu.
Kama tulivyoonyesha wiki iliyopita kwamba safari yetu ya kufuzu kwa mashindano hayo ni kama imemalizika hata kabla ya timu yetu kugusa mpira, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo wanabeba jukumu zito ambalo ni kama kupanda mlima mrefu ili kubadili matokeo.
Tunaliona ni jukumu zito kwa Stars kuzikabili Misri, Nigeria na Chad ilizopangwa nazo Kundi G la mashindano ya Afcon, ambayo mechi zake zinaanza miezi miwili ijayo.
Kwa upande wa CHAN, Stars inakutana na Uganda Cranes, timu ambayo licha ya kutoka ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kati, lakini ina rekodi ya muda mrefu ya kuionea Stars kila zinapokutana, iwe kwenye mashindano au mechi za kirafiki.
Mashindano ya CHAN yanayofanyika Rwanda, Januari mwakani, tunaamini yangekuwa nafasi nzuri yetu kuwapa nafasi wachezaji wetu, wakiwamo chipukizi ambao wamefanya vizuri kwenye Ligi Kuu inayokaribia ukingoni.

Advertisement

0 comments:

 
Top