Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), imesema vifaa BVR kits 2,098
zitatumika katika uandikishaji wa wapiga kura katika daftari la kudumu
la wapiga kura katika mikoa minne.
Nec ilisema tarehe ya Kura ya maoni itatangazwa baadaye baada ya kushauriana na Tume ya Uchaguzi zanzibar Zec
Mikoa hiyo ni Iringa, Ruvuma, Mtwara na Lindi ambayo kwa mujibu wa Takwimu zilizotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu
(NBS), itakuwa na jumla ya watu wenye sifa za kupiga kura hadi siku ya Uchaguzi Mkuu ni 2,599,205.
Mwenyekiti wa Nec, Jaji
Mstaafu Damian Lubuva (pichani), alisema vifaa hivyo ni 250
vinavyotumika kwenye uandikishaji mkoani Njombe, 248 vilivyowasili hivi
karibuni na 1,600 vinavyotarajiwa kuwasili wakati wowote.
“Vifaa hivyo kwa pamoja vitawezesha uandikishaji kwenye mikoa hiyo
kufanyika kwa haraka na kadri tutakavyoendelea kupokea vifaa ambavyo
serikali imeshavilipia vitakwenda kwenye mikoa hiyo.
Alisema kwa sasa BVR kits 250 zinatumika kwenye mkoa wa Njombe na uandikishaji utamalizika Aprili 18, mwaka huu.
Jaji Lubuva alisema wakati wowote kuanzia leo Nec itatoa ratiba
kamili ya uandikishaji kwenye mikoa hiyo, ili kuwarahisishia wananchi
kufika kwenye vituo kulingana na ratiba.
Hivi karibuni, Nec ilitangaza kusongezwa mbele kwa tarehe ya kura
ya maoni kwa Katiba inayopendekezwa kutokana na kile kinachoonekana ni
kushindwa kuandikishwa kwa wapiga kura kwenye daftari la wapiga kura
kutokana na kukosekana kwa vifaa hivyo.
